Na Avelina Musa - Dodoma.
BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira(NEMC)limesema imefanya tafiti mbalimbali na kuandaa maandiko ya miradi ambapo limeratibu utekelezaji wa miradi ya mabadiliko ya tabianchi, kupunguza matumizi ya zebaki kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu.
Hayo yamesemwa jijini hapa leo Machi 24,2025 na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt.Immaculate Semesi wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio na mwelekeo wa Baraza hilo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita.
Dkt. Semesi amesema Utafiti huo unafanyika kuainisha ubora na viwango vinavyotakiwa kuzingatiwa katika utengenezaji wa mifuko mbadala isiyo ya plastiki ili kujua uwezekano wa mifuko hiyo kuwa na uwezo wa kuoza.
“Ajenda ya tafiti imetekelezwa katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja utafiti kuhusiana na changamoto za uchafuzi wa Mto Mara,Mmomonyoko wa fukwe za maeneo ya Coco Beach,Kunduchi Beach,Mbweni JKT Beach Club na KJ742 Navy,Fukwe za Mikadi, eneo la Msuka lililopo Pemba Kaskazini, Ghuba ya Mikindani na Manispaa ya Mtwara,”amesema.
Dkt.Semesi amesema Baraza limefanya tathmini ya hali ya mazingira kwenye maeneo yanayokumbwa na maporomoko ya ardhi katika milima ya Hanang, Manyara na Mamba Myamba iliyopo Wilayani Same – Kilimanjaro.
Aidha, Dkt.Semesi amesema NEMC imefanya jumla ya kaguzi 9,606 na malalamiko 1,483 yalishughulikiwa hasa katika eneo la kelele na mitetemo.
Hata hivyo amesema Baraza lilianzisha mfumo wa kielektroniki unaotumika kusajili hadi kuidhinishwa kwa miradi ya TAM. Kabla ya mfumo, Baraza lilikuwa linasajili takribani miradi 900 kwa mwaka na baada ya mfumo Baraza linasajili zaidi ya miradi 2,000 kwa mwaka.