TUNATEGEMEA MAFANIKIO MAKUBWA REA – BODI MPYA

MUUNGANO   MEDIA
0



 Bodi ya Nishati Vijijini (REB) inayosimamia Wakala wa Nishati Vijijini

(REA), imesema inategemea mafanikio makubwa katika kuiwezesha

Wakala hiyo kutimiza azma yake ya kuwafikishia wananchi walioko vijijini

nishati bora za umeme, mafuta na gesi.

Hayo yamebainishwa mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa Bodi hiyo,

Balozi, Meja Jenerali Mstaafu, Jacob Kingu baada ya kikao cha kwanza

cha Bodi hiyo mpya kilicholenga kutambuana na kupanga majukumu.

“Kikao chetu kimeenda vizuri, tumechagua Kamati na kupangiana

majukumu. Tunaamini na tunaahidi kuwa tutatekeleza majukumu yetu

sawasawa na Sheria iliyoanzisha Wakala wa Nishati Vijijini inavyoelekeza,”

amesema.

Aidha, Balozi Kingu amemshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu

Hassan kwa kumteua kuwa Mwenyekiti wa Bodi na amemshukuru Naibu

Waziri Mkuu ambaye pia ndiye Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Dkt. Doto

Mashaka Biteko kwa kukamilisha mchakato wa uteuzi wa Wajumbe wa

Bodi, jambo ambalo limeiwezesha kuwa Bodi kamili.

Akieleza zaidi kuhusu majukumu waliyojipangia, Balozi Kingu amesema

mapema Mwezi Machi, Bodi itakutana katika kikao cha dharura kupitia na

kujadili masuala mbalimbali ya Wakala ambayo yalikuwa yakisuburi baraka

za Bodi ili kuyatolea maamuzi yatakayowezesha utekelezaji wake kwa

manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Katibu wa Bodi hiyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa

REA, Mhandisi Hassan Saidy amepongeza Mamlaka za Uteuzi, kuteua

watu makini, hodari na wachapakazi ambao amesema ni muhimu kuwa

nao katika kuisimamia Wakala hiyo yenye majukumu makubwa

yanayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

“REA ina jukumu kubwa ambalo linagusa maisha ya watu lakini pia

linahusisha kiasi kikubwa sana cha fedha za Serikali. Kwahiyo, kuwa na

Bodi nzuri iliyosheheni watu makini, kwetu sisi ni jambo la faraja,”

amefafanua.


Mkurugenzi Mkuu, kwa niaba ya Menejimenti na Wafanyakazi wote wa

REA, ametoa ahadi ya ushirikiano kwa Bodi hiyo mpya ili kuhakikisha

malengo ya Serikali kupitia majukumu yaliyokasimiwa kwa Wakala

yanatekelezwa.

“Tunatamani kuona Watanzania wenzetu wanaoishi vijijini wanapata nishati

bora kama ilivyo kwa wenzao wanaoishi mjini,” amesisitiza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Wajumbe wa Bodi wamezishukuru

Mamlaka za Uteuzi kwa kuwaamini na kuwapa jukumu hilo kubwa la

kuisimamia REA ili kuendelea kuleta matokeo chanya.

Aidha, wamepongeza Bodi zilizotangulia kabla yao, Menejementi pamoja

na Wafanyakazi wote kwa kazi nzuri waliyofanya tangu kuanzishwa kwa

Wakala na kuahidi kuendeleza yote mazuri yaliyofanyika ili kuongeza tija.

Kikao hicho pia kilishirikisha Menejimenti ya Wakala ambapo Wakuu wa

Idara na Vitengo waliwasilisha kwa Bodi taarifa za utekelezaji wa

majukumu katika maeneo wanayosimamia kwa lengo la kuijengea Bodi

uelewa na ufahamu kuhusu Taasisi hiyo waliyopewa jukumu la kuisimamia.

Januari 26 mwaka huu, Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa

Nishati, Dkt. Doto Biteko aliwateua Florian Otman Haule, Lucas Charles

Malunde, Mwantum Issa Sultan, Stephen Menard Mwakifamba, James

Issack Mabula, Ahmed Martin Chinemba, Sophia Shaban Mgonja na Balozi

Radhiya Naima Msuya kuwa Wajumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini,

wakiungana na Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Gideon Kingu

aliyeteuliwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Septemba 2023

kuwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo.

CAPTIONS

PIC 1

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi, Meja Jenerali Mstaafu

Jacob Gideon Kingu (katikati-waliokaa), akiwa katika picha ya pamoja na

Wajumbe wapya wa Bodi hiyo baada ya kikao chao cha utambulisho na

kupanga majukumu kilichofanyika hivi karibuni katika Ofisi Ndogo za

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) zilizopo jijini Dar es Salaam.

PIC 2


Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Balozi, Meja Jenerali Mstaafu

Jacob Gideon Kingu (katikati-waliokaa) na Wajumbe wapya wa Bodi hiyo,

wakiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Wakala wa Nishati

Vijijini (REA) baada ya kikao chao cha utambulisho na kupanga majukumu

kilichofanyika hivi karibuni katika Ofisi Ndogo za REA zilizopo jijini Dar es

Salaam.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)