MAKAMU WA RAIS AFUNGUA KONGAMANO LA LUGHA ZA ASILI

MUUNGANO   MEDIA
0



 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. Philip Mpango

ametoa wito kwa washiriki wa Kongamano la lugha za asili kujielekeza katika

kupanga mikakati itakayohakikisha Kiswahili na lugha nyingine za asili zinapata

fursa katika uchumi wa kidijiti ili kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika

sekta hiyo.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa

la Dhima ya Lugha za Asili katika kuendeleza Diplomasia ya Kiuchumi na

Kiutamaduni lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Four Points by Sheraton

Jijini Dar es salaam. Amesema Kongamano hilo linapaswa kuangazia namna

ambavyo Kiswahili pamoja na lugha nyingine za asili za Afrika zitakavyotumika

kuendeleza teknolojia za asili, kuchochea uvumbuzi, uwekezaji na kukua kwa

diplomasia.

Aidha Makamu wa Rais amesema Kongamano hilo linapaswa kusaidia kuonesha

fursa zilizopo katika matumizi ya lugha za asili ili kuwafanya vijana kujipatia stadi

na maarifa mbalimbali katika kujiandaa kwa mabadiliko makubwa ya kiuchumi na

kiteknolojia ndani na nje ya bara la Afrika.

Makamu wa Rais amesema kupitishwa kwa Kiswahili kuwa lugha rasmi katika

Umoja wa Afrika (AU) na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika

(SADC), kumepanua wigo wa matumizi ya Kiswahili na kuleta fursa mbalimbali za

kiuchumi na kiutamaduni. Amesema Kongamano hilo ni muhimu kubeba jukumu

kubwa la kuibua fursa zaidi na kuendeleza historia ndefu ya Kiswahili katika

kujenga uhusiano kati ya watu wa tamaduni, lugha na misingi mbalimbali ya

kiuchumi na kijamii.

Amesema Katika muktadha wa ukuaji na maendeleo ya Kiswahili, ikiwa ni pamoja

na kuhifadhi lugha nyingine za asili, tamaduni na mifumo ya maarifa asili, katika

Afrika Mashariki na Kati, wafanyabiashara wadogo na wanaoinukia

“Wamachinga” wametoa mchango ambao hauna budi kutambuliwa na

kuthaminiwa. Amesema lipo hitaji la kufanya utafiti wa kina ili kuona jinsi nchi za

Kiafrika zinavyoweza kuendeleza mifumo inayozingatia ushiriki wa vijana na

makundi kama ya wafanyabiashara waliojiajiri katika diplomasia ya kiuchumi na

kukuza biashara.


Halikadhalika Makamu wa Rais amesema Tanzania imeweka kipaumbele katika

kukuza lugha ya Kiswahili, ambapo inalenga kuifanya lugha hiyo kuendelea kuleta

umoja, amani na kuvumiliana katika bara zima la Afrika. Amekipongeza Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam kwa kuendelea kushirikiana na Vyuo na Taasisi za nje

katika kukuza Kiswahili na kuendeleza diplomasia ya kiutamaduni.

Kongamano hilo limehudhuriwa na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Msumbiji Mhe.

Joackim Chissano, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta,

Wanadiplomasia, Watunga sera, Wafanyabiashara na wenye Viwanda, Viongozi

wa Dini, Wanataaluma na Wakuu wa Taasisi za Utafiti, Vijana, Wanawake na

wawakilishi wa mashirika mbalimbali ya kiraia. Kongamano limeandaliwa na Chuo

Kikuu Cha Dar es salaam kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Kwazulu Natal cha

Afrika Kusini

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

20 Februari 2024

Dar es salaam.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)