SERIKALI YASEMA UKUTA KUJENGWA NUNGWI KUKABILI MABADILIKO YA TABIANCHI

MUUNGANO   MEDIA
0



 Serikali imesema imeanza hatua za kujenga ukuta katika eneo la Nungwi

Zanzibar kwa ajili ya kusaidia kuzuia maji ya bahari kuingia kwenye makazi

kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis

Hamza Khamis amesema hayo wakati akijibu maswali bungeni jijini Dodoma

leo Februari 01, 2024.

Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Nungwi Mhe. Simai Hassan Sadiki

aliyetaka kujua kama eneo hilo limekidhi vigezo vya kujengewa ukuta

kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mhe. Khamisi alisema kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais

inatekeleza miradi ya ujenzi wa kuta katika fukwe mbalimbali za bahari

Tanzania Bara na Zanzibar.

“Eneo ambalo linapaswa kujengwa ukuta limekidhi vigezo na lina kila sababua

ya kufanyiwa hivyo, tumeanza kufanya utafiti na ndio maana viongozi wa SMT

na SMZ wamekwishafika pale na tumeombea bajeti hivyo Serikali ina kila

sababu ya kulifanyia kazi eneo hilo,“ alisema.

Akijibu swali la msingi la mbunge huyo, Naibu Waziri Khamis alisema kuwa

Serikali itaendelea kubaini maeneo yenye changamoto kubwa ya uharibifu wa

mazingira na kuyaweka katika kipaumbele ili kuyatafutia rasilimali fedha kwa

ajili ya kuitatua.

Akiendelea kujibu swali hilo amesema kuwa mabadiliko ya tabianchi yanazidi

kusababisha athari katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo ya ukanda wa

pwani nchini.

Katika kubainisha maeneo yaliyoathirika na kuyaweka katika vipaumbele,

alisema Serikali inafanya tathmini ya kiwango cha uharibifu na athari

zitakazojitokeza hii ni moja ya sababu ya mojawapo ya vigezo vinavyotumika

kuweka vipaumbele maeneo yaliyoathirika katika mipango ya utekelezaji

Kwa upande mwingine alitoa rai kwa wananchi kuacha kufanya shughuli

zinazoharibu mazingira ya visiwa zikiwemo uvuvi usio endelevu na kilimo cha

mwani kinachoharibu mazingira

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)