M/RAIS AFUNGUA MKUTANO WA WADAU WA AJIRA BARANI AFRIKA

MUUNGANO   MEDIA
0



 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip

Mpango amesema ili kukabiliana na changamoto za utengenezaji ajira barani

Afrika yanahitajika mageuzi na mbinu jumuishi kwa kuimarisha ushirikiano

baina ya wadau wote husika.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 7 wa

Wadau wa Kijamii wa Afrika katika masuala ya Kazi na Ajira uliyofanyika

katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere Jijini Dar es

salaam, tarehe 07 Februari 2024. Amesema linahitajika jukwaa la utekelezaji

litakalounganisha mashirika ya serikali, washirika wa ndani ya nchi, sekta

binafsi pamoja na wadau wa kimataifa ili kukabiliana na changamoto za

utengenezaji wa ajira.

Makamu wa Rais amesema nchi za Afrika zinapaswa kuongeza ujuzi na

matumizi ya teknolojia ili kuongeza tija katika uzalishaji badala ya kuona

teknolojia ni adui kwa usalama wa ajira. Amesema ujio wa Akili Mnemba

(Artificial Intelligence) utaathiri utengenezaji wa ajira kwa kupunguza ajira

ndogondogo zilizopo na kutengeneza ajira mpya hususani zinazohitaji ujuzi wa

kiufundi.

Makamu wa Rais amesema matumizi ya Akili Mnemba yanazitaka Serikali na

sekta binafsi katika bara la Afrika kutoa kipaumbele kwa kuwapa wafanyikazi

ujuzi wa juu zaidi wa kiteknolojia ili kuwawezesha kuendana na soko jipya la

ajira. Ametoa wito kwa Mkutano huo kujadili umuhimu wa mafunzo mapya

kwa wafanyakazi, kufanya uchambuzi, kutambua sekta ambazo zina

uwezekano wa kupoteza idadi kubwa ya fursa za ajira na sekta ambapo Akili

Mnemba itaongeza ajira za ujuzi wa juu. Amesema eneo moja mahususi

ambalo Akili Mnemba inaweza kusaidia kutengeneza ajira ni utafiti wa kilimo

unaolenga kuboresha aina za mbegu zenye mavuno mengi na mbegu

zinazostahimili ukame ambazo zitachochea tija kubwa na ajira za baadaye.

Halikadhalika Makamu wa Rais amesema ni muhimu kwa Mkutano huo kujadili

hatua za haraka za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na athari zake

ikiwa ni pamoja na mbinu jumuishi zinazolenga kulinda maisha ya jamii na

kuimarisha ulinzi wa mazingira dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi.

Amesema mabadiliko ya tabianchi kwa upande mwingine yana fursa nyingi

katika kutengeneza ajira Barani Afrika ikiwemo katika mchakato wa

kupunguza athari, kuna ajira ambazo zinatengenezwa hususani pale wakulima

wanapotumia kilimo hai na utafutaji na ukuzaji wa mbegu na malisho kwa

jamii za wafugaji. Vile vile, amesema katika mapinduzi ya kijani kuna fursa za

ajira zilizoundwa kwa kuweka kipaumbele kwa nishati safi hususani nishati

jua, jotoardhi, upepo na maji.


Makamu wa Rais amesema Tanzania imedhamiria kutengeneza ajira milioni 7

kati ya mwaka 2020-2025 ambapo mikakati ya utekelezaji wa lengo hilo ni

pamoja na kuboresha mazingira ya biashara, uanzishwaji wa kanda maalum

za kiuchumi katika halmashauri zote za wilaya nchini zenye miundombinu

inayohitajika kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum ili

kufanya shughuli za uzalishaji mali. Amesema mikakati mingine ni pamoja na

kutoa mafunzo na kuwaunganisha vijana na taasisi zinazotoa mikopo nafuu

ikiwemo kuanzisha programu ya Jenga Kesho Bora: Mpango wa Vijana kwa

Biashara ya Kilimo (BBT-YIA) na ile ya Sekta ya Mifugo (BBT-Live) kwa ajili ya

uzalishaji wa nyama ya ng'ombe na ufugaji wa Samaki. Pia uanzisha vituo

vilivyotengwa ambapo vijana wataweza kujifunza na kupata ujuzi wa vitendo

utakaowawezesha kujihusisha na uzalishaji pamoja na kutenga asilimia 10 ya

mapato ya kila halmashauri ya wilaya kwa ajili ya wanawake, vijana na watu

wenye mahitaji maalum.

Mkutano huo unafanyika tarehe 7-8 Februari 2024 umeandaliwa na Chama

cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa Kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Waajiri

(IOE).


Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

07 Februari 2024

Dar es salaam.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)