M/RAIS AFUNGUA MKUTANO WA MAGONJWA YA MOYO ZANZIBAR

MUUNGANO   MEDIA
0


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip

Mpango amesema jitihada inahitajika katika kutoa elimu ya magonjwa

yasioambukiza pamoja na kuzingatia mtindo bora wa maisha, mazoezi na

kufanya vipimo vya afya mara kwa mara ili kukabiliana na maradhi mbalimbali

ikiwemo magonjwa ya moyo.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa

Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo unaofanyika katika Ukumbi wa Golden Tulip

Airport – Unguja, Zanzibar. Amesema katika kukabiliana na ugonjwa wa moyo

ni muhimu wananchi kufuata njia za kujikinga zaidi ikiwemo kuacha ulevi

uliyopindukia, uvutaji sigara, tabia bwete pamoja na uzito uliyopindukia.

Ametoa rai kwa watalaamu wa afya, wasomi, vyombo vya habari pamoja na

watunga sera kushiriki katika utoaji elimu kuhusu masuala ya afya.

Aidha Makamu wa Rais amesema tafiti zinapaswa kufanyika kwa kina ili

kubaini visababishi zaidi vya magonjwa ya moyo kwa kupata taarifa zaidi juu

ya taratibu za kijamii na tabia za kiutamaduni katika mambo mbalimbali

yaliyozoeleka kufanyika barani Afrika.

Makamu wa Rais amesema Tanzania imechukua hatua mbalimbali katika

kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo magonjwa ya moyo kama

vile kuimarisha Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, kufanya tafiti za afya za

kimkakati ili kupata suluhu ya changamoto mbalimbali za kiafya zinazowakabili

wananchi pamoja na kutoa elimu ya magonjwa yasiyoambukiza na magonjwa

adimu.

Amesema Taasisi ya Moyo ya jakaya Kikwete imeendelea kuimarika ambapo

kwa sasa inafanya upasuaji kwa wagonjwa wa moyo 800 kwa mwaka ikiwemo

upausaji wa kufungua kifua (upasuaji mkubwa) ukilinganisha na wagonjwa

200 wakati ikianzishwa. Amesema zaidi ya wagonjwa laki mbili hutibiwa kwa

mwaka huku zaidi ya 2400 wakitoa mataifa mengine. Ameongeza kwamba

serikali imeweza kuokoa zaidi ya bilioni 63 kila mwaka za matibabu ya

wagonjwa wa moyo kutokana na kuimarishwa kwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya

Kikwete.

Vilevile Makamu wa Rais amesema serikali itaongeza uwekezaji katika huduma

za magonjwa ya moyo na kuandaa mipango ya awali, ubunifu, tafiti ,

mafunzo, ushirikiano, udhibiti na utoaji tiba wa magonjwa ya moyo nchini.

Mkutano huo wa siku mbili uliyoandaliwa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya

Kikwete unawakutanisha Madaktari Bingwa, wataalam na wadau wa afya,

wauguzi na watunga sera kutoka mataifa zaidi ya 40 duniani kwa lengo la

kujadiliana na kubadilishana uzoefu katika masuala mbalimbali yanayohusu

magonjwa ya moyo duniani.


Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

09 Februari 2024

Zanzibar.

 

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)