Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango amezielekeza Wizara ya Afya,

MUUNGANO   MEDIA
0




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip

Mpango amezielekeza Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais - TAMISEMI na Mamlaka

nyingine zinazohusika kuhakikisha kunakuwepo na usimamizi madhubuti wa

Mpango Jumuishi wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii ili uweze kufikia

malengo yaliyokusudiwa.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa uzinduzi wa Mpango Jumuishi wa

Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii uliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha

Mikutano cha Julius Nyerere Jijini Dar es salaam. Amesema ni lazima kuweka

mfumo mzuri wa uratibu wa shughuli za mpango huo na kuhakikisha taarifa

za utekelezaji zinapatikana ikiwemo kutumia mifano ya kidijitali.

Makamu wa Rais amewasihi wahudumu wa afya watakaopewa dhamana ya

kutekeleza jukumu hilo kuzingatia weledi na kujituma pamoja na kutoa rai

kwa jamii kuupokea mpango huo na kuthamini huduma za wahudumu wa

afya ngazi ya jamii kwa kuwapa ushirikiano wa kutosha ili kulinda na

kuboresha afya katika jamii.

Halikadhalika Makamu wa Rais amesisitiza masuala ya lishe bora na usafi wa

mazingira yasiachwe nyuma katika kutekeleza Mpango huo kama njia

mojawapo ya kujenga afya na kudhibiti magonjwa ambayo yanatokana na

uchafuzi wa mazingira ikiwemo kipindupindu na malaria. Ametoa wito kwa

Jumuiya ya Kimataifa, Wadau wa Maendeleo na Wadau wengine kuunga

mkono juhudi za Serikali pamoja na vipaumbele vya Mpango huo

vilivyoainishwa wakati wote wa utekelezaji.

Vilevile Makamu wa Rais amewasihi viongozi wote wanaohusika katika ngazi

zote kuhakikisha zoezi la kuwachagua Wahudumu wa afya ngazi ya jamii

linafanyika kwa kufuata vigezo na taratibu zilizowekwa ili kupata Wahudumu

wenye sifa stahiki watakaotekeleza majukumu hayo. Amewataka

watakaopewa jukumu la kutekeleza mpango huo, kujiepusha na vitendo vya

upendeleo, rushwa au ukiukwaji wa taratibu.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita imepanga kuajiri na kuwajengea uwezo

jumla ya Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii wapatao 137,294 katika Mikoa

yote 26 ya Tanzania Bara ambapo Utekelezaji wa Mpango huo utafanyika

katika kipindi cha miaka mitano kwa awamu ambapo katika mwaka wa

kwanza (2023/24) zaidi ya Wahudumu 28,000 watafikiwa na baadaye wastani

wa Wahudumu 27,324 kila mwaka kwa kipindi cha miaka minne mfululizo

kuanzia mwaka 2024/25 hadi 2027/28. Jumla ya shilingi bilioni 899.4

zinatarajiwa kutumika katika kutekeleza mpango huo kwa kipindi cha miaka

mitano.


Kwa upande wake Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema Mpango huo

umelenga kupunguza idadi ya wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za

afya kwa kuimarisha huduma za afya kinga pamoja na kuongeza tija na

ufanisi katika kutoa huduma za afya kufikia lengo la afya kwa wote.

Ameongeza kwamba Mpango huo utasaidia kukabiliana na upungufu wa vituo

vya kutolea za afya hususani katika maeneo ya vijijini. Aidha amesema kupitia

mpango huo wahudumu wa afya ngazi ya jamii wameweza kuibua magonjwa

mbalimbali yanayoikabili jamii kama vile Kifua Kikuu, Kipundupindu na

ugonjwa wa Marburg.

Amesema kupitia mpango huo wataweza kupunguza gharama za matibabu

kutokana na kutambulika kwa ugonjwa katika hatua za awali zaidi. Amesema

umuhimu wa wahudumu hao ngazi ya jamii ni daraja kati ya vituo vya kutolea

huduma na jamii husika kwa kuwa wamekuwa wakitambua mapema maradhi

yanayojitokeza.

Waziri Ummy amesema katika kuchagua wahudumu wa afya ngazi ya jamii

suala la wakazi wa eneo husika litazingatiwa ili kuendana na mila na desturi za

wananchi wa eneo hilo.


Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

31 Januari 2024

Dar es salaam.

 

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)