Wajumbe wa Kamati ya Kitaalam ya Ushauri ya Mpango wa Taifa wa Huduma za Afya na Lishe Shuleni(TAC) wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa kuhitimisha Kikao cha kamati hiyo Mkoani Morogoro.
Kaimu Mkurugenzi wa idara ya Huduma za Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Otilia Gowelle akizungumza katika Kikao cha TAC Mkoani Morogoro.
Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma kutoka Wizara ya Afya Dkt. Ona Machangu akiwa katika Kikao cha TAC mkoani Morogoro.
Alhaji Abdul Maulid,Mkurugenzi Elimu Msingi kutoka Wizara ya Elimu akizungumza katika Kikao cha Kamati ya Kitaalam cha Ushauri wa Mpango wa Taifa wa Huduma za Afya na lishe shuleni kilichofanyika Mkoani Morogoro.
Na.Mwandishi Wetu.
Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya Kitaalam cha Ushauri cha Mpango wa Taifa wa Huduma za Afya na Lishe Shuleni(TAC) wamependekeza kuimarisha uratibu wa Klabu za Afya na lishe shuleni kwa kuzingatia muongozo wa Uanzishaji na Uendeshaji wa Mabaraza ya Watoto.
Wakizungumza mkoani Morogoro katika Kikao cha Kamati ya Kitaalam cha Ushauri wa Mpango wa Taifa wa Huduma za Afya na lishe shuleni wajumbe hao wamesema uimarishaji wa Klabu hizo kutasaidia kwa kiwango kikubwa katika utekelezaji wa afua na lishe shuleni.
Kwa mujibu wa Tathmini iliyofanyika hivi karibuni mkoani Morogoro katika shule za msingi na sekondari wilaya za Ifakara na Gairo, kila shule ina muongozo wake ambao unaandaliwa ama na wadau, shule zenyewe na hata halmashauri, hivyo kutofautiana kati ya mmoja na mwingine.
"Haya si maelekezo ya Wizara, hivyo tujipange ili shule ziwe na klabu ambazo maudhui yake yameidhinishwa na Serikali," amefafanua Mwenyekiti wa kikao hicho, Dkt. Otilia Gowelle.
Kikao hicho kinachoendelea leo mkoani Morogoro ikiwa ni siku ya pili kitatoka na maazimio yatakayowezesha kutekeleza mpango huo kwa ufanisi.
Wizara za Kisekta zilizokutana ni Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Wizara ya Elimu, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Mifugo na Wizara ya Afya.