M/RAIS AFUNGUA MKUTANO WA 21 WA TAASISI ZA FEDHA ARUSHA

MUUNGANO   MEDIA
0



 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip

Mpango ametoa wito kwa washiriki wa Mkutano wa 21 wa Taasisi za Fedha

kutafakari kwa kina changamoto ya uhaba wa fedha za kigeni na hatua gani

za muda mfupi na wa kati zinazopaswa kuchukuliwa zaidi ya hatua za urekebu

zinazochukuliwa na Benki Kuu ya Tanzania.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa

Taasisi za Fedha unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha

(AICC). Amesema ni muhimu kwa Mkutano huo kujadili nafasi ya kutumia

viwango nyumbufu vya ubadilishanaji fedha (exchange rate flexibility) katika

kudhibiti uhaba huo wa fedha za kigeni.

Aidha Makamu wa Rais amewataka viongozi na wataalam katika sekta ya

fedha nchini kuhakikisha uwezo wa taasisi zao na sekta nzima unaimarika

zaidi ili kuhimili misukosuko inapotokea. Amewasihi kuangalia namna ya

kuimarisha zaidi Idara na vitengo vya utafiti na masoko ya kifedha nchini.

Amesema Menejimenti ya vihatarishi, usimamizi makini na ufuatiliaji wa

mwenendo wa benki moja moja na sekta nzima ni jambo la muhimu sana

katika kujenga sekta ya fedha iliyo imara na yenye uwezo wa kuhimili

misukosuko.

Halikadhalika Makamu wa Rais amesema Mkutano huo unapaswa kuangazia

njia za kudhibiti mikopo chechefu, kupunguza gharama za mikopo na kupanua

wigo wa mikopo nafuu hasa kwa wajasiriamali wadogo na wa kati katika sekta

za kilimo, mifugo, uvuvi, uchimbaji wa madini na viwanda vidogo. Pia

amesema sekta ya fedha inao wajibu wa kushiriki katika jitihada za kuhifadhi

mazingira na kudhibiti athari za mabadiliko ya tabianchi kwani huathiri

uzalishaji na mapato hususan katika sekta ya kilimo, utalii, ufugaji na hata

uzalishaji katika viwanda vinavyotegemea malighafi zinazotokana na kilimo,

misitu na maliasili.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa taasisi zote za fedha kuimarisha jitihada za

kudhibiti madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukuaji wa kasi wa

teknolojia ikiwa ni pamoja na changamoto za utunzaji na usiri wa taarifa,

usalama wa mtandao wa kibenki, usambazaji wa taarifa potofu mitandaoni,

udhibiti wa fedha haramu pamoja na kuwalinda watumiaji kwa kushirikiana kwa

karibu na wadau wote.


Vilevile Makamu wa Rais amesema sekta ya fedha nchini kwa kiwango cha

kuridhisha imeweza kuhimili misukosuko ya kiuchumi iliyojitokeza katika miongo

miwili iliyopita na kupata mafanikio mazuri. Amesema takwimu rasmi za

maendeleo ya sekta ya fedha nchini na tathmini ya Shirika la Fedha la Kimataifa

(IMF) ya Disemba 2023 vinathibisha hivyo. Ametaja kwamba sekta kibenki iko

imara na ina mtaji na ukwasi wa kutosha huku inatengeneza faida. Ukuaji wa

mikopo iliyotolewa na mabenki kwa sekta binafsi umeongezeka kutoka 9.9%

mwaka 2021/22 hadi 22.2% mwaka 2022/23. Halikadhalika, uwiano wa mikopo

kwa sekta binafsi na Pato la Taifa ulifikia wastani wa 18.2% katika mwaka

2021/22 ikilinganishwa na 17.6% mwaka 2020.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Hamad Chande amesema

Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeendelea kutekeleza jukumu muhimu

katika juhudi za kuimarisha sekta ya fedha kulingana na mpango mkuu wa

maendeleo ya sekta ya fedha wa mwaka 2020/2021-2029/2030. Pia amesema

Wizara ikiwa msimamizi mkuu wa sera za kiuchumi inashirikiana kwa karibu

na wadau wa sekta ya fedha kuendeleza hatua zinazokusudia kuimarisha

sekta ya fedha kwa kutunga na kutekeleza sera zinazoboresha mazingira ya

udhibiti, kuimarisha mfumo wa viashiria hatarishi na kukuza uwezo wa ndani

wa sekta ya fedha.

Aidha Chande ameongeza kwamba Sekta ya Fedha ya Tanzania imeonesha

uvumilivu katika kupambana na changamoto za uchumi wa dunia za hivi

karibuni. Amesema ufanisi huo unajionesha katika ukuaji wa rasilimali hasa

mikopo kwa sekta binafsi ambayo iliweza kukua kutokana na teknolojia za

kifedha za hali ya juu na hatua zilizochukuliwa na Serikali pamoja na Benki

Kuu za kuimarisha uchumi wa Taifa.

Akizungumzia uzinduzi wa Mfumo wa Taifa wa Malipo ya Papo kwa Hapo

(Tanzania Instant Payments System) Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania

Emmanuel Tutuba amesema uzinduzi wa mfumo huo unathibitisha dhamira ya

serikali ya awamu ya sita ya kutumia ipasavyo mifumo ya kielektroniki katika

kurahisisha mazingira mazuri ya biashara, kuongeza ufanisi katika utendaji

kazi na kupunguza gharama na muda katika kufanya malipo.

Ameongeza kwamba Katika kutekeleza adhma ya serikali, Benki Kuu ya

Tanzania imeendelea kusimamia mifumo ya malipo kwa wadau mbalimbali

pamoja na kudhibiti viatarishi mbalimbali vinavyoweza kujitokeza kupitia

mifumo ya malipo. Amesema Benki Kuu ya Tanzania imeweza kufanya ubunifu


wa kutengeneza mfumo huo wa TIPS ambao umezingatia viwango vya

kimataifa katika kutoa huduma kwa wananchi na kuwezesha ufanyaji miamala

ya kifedha kwa haraka na kwa gharama nafuu zaidi.

Mkutano huo wa unafanyika tarehe 07-08 Machi 2024 kwa kauli mbiu isemayo

“Kuimarisha Uwezo wa Sekta ya Fedha kuhimili misukosuko ya kiuchumi”.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)