M/RAIS ASHIRIKI IBADA YA WAKFU KWA ASKOFU MOLLEL ARUSHA

MUUNGANO   MEDIA
0


 Mhe. Askofu Dkt. Alex Malasusa, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri

Tanzania;

 Mhe. Askofu Dkt. Fredrick Shoo, Mkuu wa KKKT Mstaafu na Askofu wa

Dayosisi ya Kaskazini;

 Mhe. Askofu Dkt. Abel Godson Mollel, KKKT Dayosisi ya Kaskazini Kati;

 Mhe. Askofu Mstaafu Dkt. Solomon Massangwa, KKKT Dayosisi ya Kaskazini

Kati;

 Wahe. Maaskofu wote wa KKKT mliopo;

 Wahe. Maaskofu na Viongozi wa Madhehebu mengine ya Kikristo;

 Sheikh Shaban Juma, Sheikh wa Mkoa wa Arusha;

 Mhandisi Robert Kitundu, Katibu Mkuu KKKT;

 Mch. Canon Dkt. Moses Matonya, Katibu Mkuu Jumuiya ya Kikristo Tanzania;

 Mch. Lareiton Lukumay – Msaidizi wa Askofu KKKT Dayosisi ya Kaskazini Kati

na Wasaidizi wote wa Maaskofu;

 Makatibu wa Dayosisi za KKKT;

 Wageni wote wa KKKT kutoka nje ya nchi;

 Wachungaji na Wainjilisti;

 Wenza wa Maaskofu;

 Waheshimiwa Mawaziri mliopo;

 Mhe. John Mongela, Mkuu wa Mkoa wa Arusha;

 Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Mkoa wa Manyara;

 Wahe. Wakuu wa Wilaya wote mliopo;

 Mhe. Mrisho Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini na Wahe. Wabunge

wengine mliopo;

 Viongozi wengine wote wa Serikali mliopo hapa;

 Wapendwa waumini wa KKKT;

 Waandishi wa habari, Mabibi na mabwana

Bwana Yesu asifiwe...

Utangulizi

Mhe. Mkuu wa Kanisa, Maaskofu, Wachungaji na Waamini wote wa KKKT;

1. Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha

kujumuika katika ibada hii maalum. Pili, nalishukuru Kanisa la Kiinjili la Kilutheri

Tanzania kwa kukubali nimwakilishe Mhe. Rais na Serikali katika ibada hii

maalum. Nafahamu kwamba Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri

ya Muungano wa Tanzania ndiye mliyemwalika kuwa Mgeni rasmi katika ibada

hii. Lakini kutokana na kuzongwa na majukumu mengi ya kitaifa, amenituma

kumwakilisha.

2. Pamoja na tukio la leo, mwezi Januari, 2024 ilifanyika ibada maalum ya

kumuingiza kazini Mhe. Askofu Dkt. Malasusa kuwa Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la

Kilutheri Tanzania. Napenda kutumia fursa hii kukupongeza sana Mhe. Askofu

Dkt. Malasusa kwa kuitwa na kukubali kutumikia tena katika nafasi ya Mkuu wa


3


KKKT. Tunakuombea kwa Mungu ili akuongoze katika kutekeleza majukumu

hayo mazito; maana yeye hatakuacha kama alivyoahidi katika Kitabu cha Nabii

Isaya, “Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana

mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika

kwa mkono wa kuume wa haki yangu.” (Isaya 41:10)

3. Napenda pia kutumia nafasi hii kumpongeza sana Mhe. Askofu Dkt. Shoo

ambaye alikuwa Mkuu wa KKKT kwa kipindi cha miaka 8 iliyopita. Serikali

inakupongeza Mhe. Askofu Shoo kwa kuliongoza Kanisa vema na kuendeleza

mahusiano mema na Serikali hadi ulipomaliza kipindi chako cha Mkuu wa

Kanisa. Serikali inakutakia heri katika Nimetaarifiwa kuwa ingawa umekabidhi

majukumu ya ukuu wa Kanisa, bado unaendelea kuwa Askofu na kiongozi wa

Dayosisi ya Kaskazini. Hivyo, Baba Askofu Dkt. Shoo nakupongeza sana na

ninakutakia baraka na heri katika kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu

katika nafasi yako ya Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini.

4. Kwa namna ya pekee, ninaleta kwa Mhe. Askofu Dkt. Abel Godson Mollel na

Msaidizi wako Mch. Lareiton, pongezi za dhati kutoka kwa Mhe. Samia Suluhu

Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchaguliwa kuongoza

Dayosisi hii ya Kaskazini Kati. Hatuna mashaka kuwa mtatekeleza kwa haki na

uchaji wa Mungu majukumu mliyokabidhiwa leo. Mungu mwenyewe

atawawezesha na kuwaongoza. Kama tunavyosoma katika kitabu cha Yeremia

33.3 aliahidi kwamba “Niite, nami nitakuitikia, nami nitakuonesha mambo

makubwa, magumu usiyoyajua”.

5. Aidha, ninatoa pongezi nyingi kwa Mhe. Askofu Dkt. Massangwa –aliyekabidhi

uongozi wa Dayosisi hii ya Kaskazini kati. Nimepewa taarifa kwamba yeye

alipokea Dayosisi katika mazingira tofauti kwani hakupata nafasi ya kukabidhiwa

na mtangulizi wake, Mhe. Hayati Askofu Dkt. Thomas Laizer. Pamoja na

mazingira hayo, kwa msaada wa Mungu alisimama imara na kwa kipindi cha

miaka kumi aliendeleza kwa umahiri kazi ya uinjilishaji. Hongera sana Mhe.

Askofu Massangwa, bila shaka Mungu unayemtumikia atakulipa kwa utumishi

wako kama ilivyoandikwa katika 1 Petro 5:4 kwamba “Na Mchungaji Mkuu

atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka”. Zaidi ya hayo,

nakutakia maisha mema ya uzee, ukafurahi na wajukuu huku ukiendelea kutoa

ushauri kwa Mhe. Askofu Mollel watumishi wengine.

6. Naomba kutumia nafasi hii kuwakumbusha Waamini wa Dayosisi hii na Wakristo

wote kuhusu wajibu wetu kwa Viongozi wetu wa kiroho. Waraka wa Timotheo

unatukumbusha kuwa: “Viongozi wa Kanisa wanaowaongoza watu vizuri

wanastahili kupata heshima mara dufu, hasa wale wanaofanya bidii katika

kuhubiri na kufundisha” (1 Tim 5:17). Aidha, Mtume Paulo anatuasa kuwa:

“Watiini viongozi wenu na kushika amri zao. Wao huchunga roho zenu usiku na

mchana, watatoa ripoti ya utumishi wao mbele ya Mungu. Kama mkiwatii

watafanya kazi kwa furaha, la sivyo watazifanya kwa huzuni na hiyo haitakuwa

na faida kwenu” (Waebrania 13:17). Nawaomba sana waamini wenzangu


4


kumpa Mhe. Askofu Dkt. Abel ushirikiano wa dhati ikiwa ni pamoja na

kumpenda, kumtii, kumtia moyo na kumwombea kwa Mwenyezi Mungu. Hivyo

hivyo, naiomba familia ya Mhe. Askofu Mpya, hususan Mke wake kumtunza,

kumpenda, kumsaidia na kuzidi kumwombea ili aweze kutenda kazi yake pasipo

vikwazo vya aina yoyote nyumbani.

Mhe. Mkuu wa Kanisa, Maaskofu, Wachungaji na Waamini wote wa KKKT;

7. Napenda kutumia hadhara hii kuwahakikishia kuwa, Serikali inayoongozwa na

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, itahakikisha kuwa wakati wote itasimamia na

kulinda haki ya kuabudu kwa wananchi wote bila ubaguzi. Aidha, itahakikisha

kwamba wananchi wanaendelea kuishi kwa amani na kupata huduma bora za

kijamii. Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi mikubwa ya kimkakati katika

sekta zote, ambayo ikikamililika itachangia kwa kiasi kikubwa kuinua uchumi wa

Taifa letu. Nawaomba viongozi wa KKKT na madhehebu mengine kuendelea

kuiunga mkono Serikali ili kwa pamoja tuweze kumhudumia Mtanzania kimwili

na kiroho kama iwapasavyo watoto wa Mungu.

8. Kama mnavyofahamu, mwaka huu utafanyika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Uchaguzi huu ni muhimu kwa kuwa utatupatia viongozi katika mashina

wanakoishi wananchi kwa ajili ya kuchochea maendeleo na ustawi wa jamii.

Nawaomba viongozi wote wa dini nchini kusaidia kutoa hamasa kwa wananchi ili

wajitokeze kwa wingi kushiriki katika uchaguzi huo. Serikali inaahidi kufanya

jitihada za kuweka mazingira ya haki na wezeshi ili wananchi waweze kushiriki

kuchagua viongozi wanaowataka kwa amani na utulivu.

Mhe. Mkuu wa Kanisa, Maaskofu, Wachungaji na Waamini wote wa KKKT;

9. Serikali inajivunia ushirikiano mzuri uliopo kati yake na taasisi za dini ambao

umedumu kwa muda mrefu katika nyanja mbalimbali na inatambua na

kuthamini mchango mkubwa wa Kanisa katika utoaji wa huduma za jamii,

hususan elimu, afya na maji. Nimesikia ombi lako Mhe. Mkuu wa Kanisa juu ya

kuhuisha ushirikiano baina Serikali na la KKKT na madhehebu mengine katika

utoaji wa huduma katika hospitali ya Urkesumet na hospitali ya Selian (ALMC).

Napenda kukuahidi kwamba Serikali kupitia Wizara ya Afya itashirikiana kwa

karibu na KKKT katika kutatua changamoto zilizopo hivi sasa. Hivyo, naiagiza

Wizara ya Afya na TAMISEMI kukaa pamoja na viongozi husika katika Kanisa ili

kutafuta muafaka wa jambo hili na kuwasilisha ushauri Serikalini ili kulipatia

ufumbuzi suala hili.

Mhe. Mkuu wa Kanisa, Maaskofu, Wachungaji na Waamini wote wa KKKT;

10. Yapo mambo machache ambayo napenda kuwaomba kwa niaba ya Serikali,

myawekee msisitizo zaidi katika mafundisho na maonyo yenu ya Kimungu.

Jambo la kwanza, ni kulinda na kudumisha Amani, Umoja na Uhuru wa nchi

yetu. Tunu hizi za Taifa ndizo zinazotutambulisha sisi kama Watanzania popote

duniani. Kwa namna ya kipekee kabisa napenda kuwashukuru kwa kuendelea

kudumisha amani, umoja na uhuru wa Taifa letu. Pili, ni usafi na utunzaji wa


5


mazingira. Nawaomba Viongozi wa dini kuendelea kupaza sauti kuhamasisha

ulinzi na uhifadhi wa mazingira katika nchi yetu. Tukemee ukataji na uchomaji

hovyo wa misitu na uchafuzi wa mazingira katika maeneo mbalimbali.

Tuwahimize waamini na wananchi wote kuheshimu na kuzingatia matumizi bora

ya ardhi hususan maeneo ya kilimo, mifugo na vyanzo vya maji, na Nne,

tunatambua kuwa maendeleo hayawezi kuja bila kuwepo kwa ushirikiano.

Hivyo, nawahimiza kudumisha ushirikiano kati ya madhehebu mbalimbali ya dini

na Serikali pia.

11. Nimalizie kwa kuwapongeza tena Mhe. Askofu Dkt. Abel Mollel na Mch. Lareiton

kwa kupokea majukumu mliyopewa ya kumtumikia Mungu, na Kanisa katika

Dayosisi hii. Nawaomba wakristo wenzangu na wananchi wote tuwaombee

viongozi wetu hawa ili wadumu daima katika kumtumikia Mungu na awaepushe

na vikwazo mbalimbali.

Nawashukuru sana kwa ahadi yenu ya kuendelea kumuombea Mhe. Rais na sisi

wasaidizi wake ili tutimize vema majukumu yetu ya kuwatumikia Watanzania

kwa unyenyekevu na uchaji wa Mungu pia. Aidha, nitafikisha salamu zenu kwa

Mhe. Rais kama mlivyozitoa.

Asanteni kwa kunisikiliza.

 

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)