KATAVI KUTOPOKEA AU KUWASILISHA BAJETI YA HALMASHAULI YEYOTE ISIYO TATUA KERO ZA WANANCHI.

MUUNGANO   MEDIA
0

Mkuu wa mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko akitoa maelekezo ya serikali kuhusu utatuzi wa kero za wananchi kupitia bajeti mpya.Picha na Mary Clemence
Baadhi ya Wakuu wa idara wilaya ya Mlele wakiwa kwenye kikao cha tathmini na maandalizi ya bajeti mpya ya mwaka wa fedha 2024/2025.Picha na Mary Clemence


Katavi.Serikali mkoani Katavi  haitapokea au  kuwasilisha wizara ya Tamisemi  bajeti mpya ya halmashauri yeyote, isiyolenga kutatua kero za wananchi kwa mwaka wa fedha 2024/2025. 


Hayo ni kwa mujibu wa Mkuu wa mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko leo Jumatano Februari 14,2024   akitoa mwelekeo wa serikali katika kikao cha tathmini na maandalizi ya bajeti mpya.


Utaratibu huo umeanzishwa  ili kupata mwarobaini wa kero za wananchi zinazoibuka kwenye mikutano ya hadhara mbele ya viongozi wa kitaifa.


 “Kabla bajeti hii hatujasonga nayo mbele kutoka kwenye ngazi ya mkoa kwenda taifa, Wakurugenzi na timu  zenu  hakikisheni zinajibu matatizo  na sivinginevyo,”amesema Mrindoko akaongeza.


“Kila halmashauri ina  kero zake kutokana na mazingira, idadi ya watu, miundombinu iliyopo,itathmini upya bajeti yake hususani inayotokana na mapato ya ndani,”


Awali Afisa kilimo halmashauri ya Mlele Luke Kifyas miongoni mwa wajumbe  ametaja sababu inayochangia kutofikia lengo la ukusanyaji mapato ya ndani  ni   matamko ya kisiasa.


“Tuna ushuru wa karanga ghafi,kichele zilizomenywa,mpunga na mchele,mwaka jana tungefanya vizuri ukusanyaji mapato lakini wanasiasa walisema wananchi watatuonaje?,”


“Tulisitisha hizo tozo athari imekuja kwetu tumeshindwa kutekeleza miradi ya maendeleo kwa baadhi ya maeneo, tutilie  mkazo suala hili,”amesema Kifyasi.


Kauli hiyo ikawaibua Diwani wa kata ya Ilunde ambaye pia ni Mjumbe wa kamati ya fedha Martin Mgoloka na Soud Mbogo Mwenyekiti wa halmashauri ya Mlele wakikiri kuwepo hali hiyo.


“Tuliathirika,tumejadiliana kupitia  kamati ya fedha tumeomba kuandaliwa kikao na wadau, ushirikishwaji wananchi  mdogo, kelele zilikuwa nyingi   wadau wa biashara hawakushirikishwa,”amesema Mgoloka.  


“Tumeona hilo ndiyo maana  rasimu ya Mlele tumetoka   asilimia ishirini ya kwenda kwenye miradi ya maendeleo hadi kufikia arobaini, itakasaidia kutatua kero za wananchi tunaowasimamia,”amesema  Mbogo.


Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Takukuru wilaya ya Mlele Leonida Mushema akaibua hoja ya  kukosa ushirikiano wa kuonyesha madeni halisi yaliyopo kwenye mfumo.


“Naomba wataalam toeni vielelezo mlivyonavyo ili mlipwe hizo fedha, changamoto tunayokumbana nayo na inatuchelewesha wanaopewa kazi ya kukusanya mapato hawana mikataba,”


“Pia anapokabidhia posi hakuna kitabu kingine anachosaini wakati mwongozo unasema iandikwe, inatuathiri tunapoenda kwenye vyombo vya sheria  wanaturudisha,”amesema Leonida.


Anna John mkazi wa mkoa wa Katavi amesema  kwa bajeti ya mwaka wa fedha 2024/2025 kiu ya Wanakatavi kuona serikali inakamilisha miradi ya maendeleo.


“Wananchi wanasubiri huduma kuna ongezeko la watu  ikilinganishwa na awali, bado shule hazitoshi  na mengineyo matokeo ya sensa ni kipimo halisi cha mahitaji yaliyopo,” amesema Anna.


Kikao hicho kilichohudhuriwa na Wakuu wa idara na wilaya   kutoka halmashauri zote, kimeazimia kila mtumishi kufanya kazi kwa mujibu wa sheria ili kutimiza adhima ya serikali.


 

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)