WAZIRI MKUU: JUKUMU LA USALAMA BARABARANI NI LA KILA MTU.

MUUNGANO   MEDIA
0

 

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema kuwa jukumu la usalama barabarani ni la kila mtu na si la Serikali pekee na amewataka wananchi wote watoe ushirikiano kuzuia ajali za barabarani.

Ametoa kauli hiyo jana (Jumanne, Machi 14, 2023) wakati akizungumza na washiriki waliohudhuria uzinduzi wa Wiki ya Usalama Barabarani Kitaifa uliofanyika kwenye viwanja vya Furahisha, jijini Mwanza. 

Amesema kuwa madereva wa magari na pikipiki nao wamekuwa ni sehemu kubwa ya vyanzo vya ajali za barabarani na kuchangia kuongezeka kwa ajali kwa kuendesha kwa mwendo kasi, kuyapita magari ya mbele bila ya kuchukua tahadhari, kuendesha magari mabovu ama kutoheshimu alama na michoro ya barabarani.

Katika kuhakikisha ushirikiano miongoni mwa wadau unakuzwa na mapambano dhidi ya ajali za barabarani yanaimarishwa, Waziri Mkuu ameliagiza Baraza la Taifa la Usalama Barabarani liharakishe mchakato wa mapendekezo ya marekebisho ya sheria na kanuni za usalama barabarani ili kuwe na sheria bora isiyoacha mwanya kwa watumiaji wa barabara na waendesha vyombo vya moto.

Mapema, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo, Jumanne Sagini alisema makosa ya kibinadamu ndiyo yanaongoza kwa kuchangia ajali nyingi za barabarani, na kwamba Baraza linaandaa mkakati ambao ni shirikishi na unaolenga kuwadhibiti madereva walevi na wanaoendesha kwa uzembe.

Naye, Inspekta Jenerali wa Polisi, Camillus Wambura alisema maadhimisho ya wiki ya usalama barabarani yatumike kama chachu ya kuwakumbusha Watanzania kwamba kila mmoja anapaswa kuchukua tahadhari awapo barabarani. ”Maadhimisho haya yanatukumbusha kuwa sote ni wahanga wa barabara, kwa hiyo tunahitaji kuchukua tahadhari za usalama tuwapo barabarani.”
 
Maadhimisho ya Wiki ya Usalama Barabarani yalianza jana Machi 13 na yanatarajiwa kuhitimishwa Machi 19, mwaka huu. Kaulimbiu ya mwaka huu inasema: “Tanzania bila ajali za barabarani inawezekana, timiza wajibu wako.”
Tags

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)