Na Avelina Musa - Dodoma.
SHIRIKA la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika mwaka huu wa fedha limepanga kuanzisha vituo vya gesi asilia mikoa ya Pwani, Morogoro na Dodoma.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano TPDC Bi.Marie Msellemu,ameyasema hayo leo Agosti 6,2024 wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye banda la TPDC katika maonyesho ya Wakulima Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.
Amesema kuwa hatua hiyo itasaidia mtu kusafiri kufsafiri kutoka Dar hadi Dodoma kwa kutumia gesi asilia kwasababu ni rafiki kwa mazingira.
“Vituo hivyo vitasaidia mtu kusafiri kutoka Dar es salaam hadi Dodoma kwa usafiri unaotumia gesi asili. Usafiri huu ni mzuri na salama kwasababu hautumii gharama kubwa na ni rafiki kwa mazingira,”amesema.
Kwa upande wake Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Mbeya Sophia Mwakagenda,ameipongeza serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi.
Amesema serikali imeendelea kutenga bajeti kwa ajili ya kujenga vituo vya kujazia gesi asilia ili kurahisisha upatikanaji wa huduma hiyo Kwa wananchi.
Mwisho.