MA DC WAJENGEWA UWEZO KUSIMAMIA UTOAJI WA MIKOPO YA ASILIMIA 10

MUUNGANO   MEDIA
0

 


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais - TAMISEMI Bw. Sospeter Mtwale

amesema Wakuu wa Wilaya wanapatiwa mafunzo na Ofisi ya Rais -

TAMISEMI ya kuwajengea uwezo wa kusimamia zoezi la utoaji na

urejeshaji wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri za Wilaya

kwa akina mama, vijana na wenye ulemavu.


Bw. Mtwale amesema hayo leo katika Ukumbi wa Shule ya Uongozi ya

Mwalimu Julius Nyerere Kibaha mkoani Pwani kwa Niaba ya Katibu Mkuu,

Ofisi ya Rais - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru wakati akifungua kikao kazi

cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI Mhe. Mohamed Mchengerwa

na Wakuu wa Wilaya zote nchini.


Bw. Mtwale amesema, Serikali imeanza kutoa mikopo ya asilimia 10 baada

ya hapo awali kusitishwa kutokana na changamoto jilizojitokeza, na

kuongeza kuwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeshapitia kanuni na kufanya

maboresho na ikaona ni vema Wakuu wa Wilaya wakapitishwa katika

kanuni hizo ili waweze kushiriki kikamilifu katika usimamizi wa utoaji wa

mikopo hiyo.


“Tumeona ni vema nanyi mkapitishwa katika kanuni hizo ili tuwe na uelewa

wa pamoja katika kusimamia utoaji wa mikopo hiyo ili mikopo hiyo iwe na

tija kwa watakaonufaika na katika taifa kwa ujumla,” Bw. Mtwale

amesisitiza.


Sanjali na hilo, Bw. Mtwale amesema Wakuu wa Wilaya watapitishwa

katika taarifa ya ukaguzi ya mwaka wa fedha 2022/23 ili wafahamu hoja

zilizoibuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwani

nao ni wasimamizi wa halmashauri zilizopo katika maeneo yao ya utawala.


Ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Wakuu wa Wilaya

nchini, Bw. Mtwale amesema Ofisi ya Rais - TAMISEMI imemualika

mtaalamu wa afya ya akili kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Dkt.

Garvin Kweka ili kuwapatia elimu ya afya ya akili na ya namna bora ya

kuepukana na magonjwa ya afya ya akili.


Akiwasilisha mada kuhusiana na afya ya akili, mtaalamu wa afya ya akili

kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Dkt. Garvin Kweka amewataka

Wakuu wa Wilaya kuzingatia mahusiano ya kijamii ili kujenga afya nzuri ya

akili itakayowawezesha kutekeleza kikamilifu majukumu yao kwa ufanisi.


“Mtu anayeenda kwenye jumuiya, vikoba, kanisani au msikitini akipata

msiba, msiba wake hauwi sawa na mtu anayejifungia ndani hivyo

mahusiano ya kijamii ni lazima yazingatiwe na kisingi ndio utulivu wa afya

ya akili,” Dkt. Kweka amesisitiza.


Kikao kazi hicho cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI Mhe.

Mohamed Mchengerwa na Wakuu wa Wilaya zote nchini, chenye lengo la

kuwajengea uwezo kiutendaji viongozi hao kinafanyika kwa siku mbili

katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopo Kibaha mkoani

Pwani.

Tags

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)