MWEGOHA AONGOZA WANAMZUMBE KUMUAGA MAREHEMU BALOZI DKT. KAMALA

MUUNGANO   MEDIA
0



 Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Prof. William Februari 17, 2024 katika

Parokia ya Mwenyeheri Isidori Bakanja, Boko - Dar es Salaam ameungana na

ndugu, jamaa na marafiki, katika kuuaga mwili wa Balozi Dkt. Diodorus Buberwa

Kamala aliyefariki dunia tarehe 12 Febuari 2024.

 

Prof. Mwegoha amewasilisha salamu za pole kutoka kwa Mkuu wa Chuo Kikuu

Mzumbe na Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Dkt. Ali

Mohamed Shein, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo, Prof. Saida Yahya – Othman,

ambao kwa pamoja wamemwelezea Marehemu Balozi Kamala kama kiongozi

aliyekuwa na maono ya kimkakati katika kuimarisha uhusiano wa kimataifa ndani na

nje ya nchi, kujenga amani na kuleta maendeleo kwa Tanzania kupitia nyadhifa

mbalimbali alizoshika enzi za uhai wake.

 

“Tukio hili si jepesi kulipokea hasa ukizingatia mahusiano mema ambayo marehemu

aliyejenga na wafanyakazi wenzake, wanafunzi na watu mbalimbali waliobahatika

kukutana naye. Pia, ni pigo kubwa kwa jamii yetu na kwa nchi ya Tanzania kwa

ujumla kupoteza kiongozi mwenye uzoefu na mchango mkubwa katika nyanja

mbalimbali hususan kwetu sisi wanataaluma” Amesisitiza Prof. Mwegoha

 

Amesema Balozi Dkt. Diodorus Buberwa Kamala atakumbukwa sana kwa mchango

mkubwa kwa Chuo Kikuu Mzumbe toka alipokuwa Rais wa Serikali ya Wanafunzi

(IDM-Mzumbe), akiwa mtu aliyeipenda sana kazi yake katika kuongoza kundi kubwa

la wanachuo na kuajiriwa kama Mkufunzi mwenye ufahamu wa hali juu katika

masuala ya Uchumi.

 

“Mchango wa Balozi Dkt. Diodorus Buberwa Kamala bado unaishi na utaendelea

kuishi kupitia kazi nyingi za kitaaluma na kisiasa alizozifanya. Moja ya vitu

vinavyofariji ni sifa aliyokuwa nayo ya kupenda kuyaweka mawazo yake katika

maandishi. Hii inatusaidia kubaki na rejea ya mambo aliyoyafahamu, vitu

alivyoviamini na mawazo aliyoyajenga juu ya mambo mbalimbali” Amesisitiza Prof.

Mwegoha. 

 

Awali, Paroko wa Kanisa la Mwenyeheri Isidori Bakanja Padri Emmanuel Makusalo

na Padri Florence Rutaihwa Rwehumbiza kutoka Baraza la Maaskofu Tanzania

walioendesha ibada ya misa ya mazishi, kwa pamoja, wamewataka waamini na

waombolezaji kujiandaa na kifo kwa kudumu katika sala ili waweze kukikabili vema

kwa kuwa hakuna ajuaye siku wala saa.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)