UTPC YAZINDUA OFISI ZAKE JIJINI DODOMA.

MUUNGANO   MEDIA
0

 

Na. Gideon Gregory, Dodoma.

Umoja wa waandishi wa habari Tanzania (UTPC) umezindua ofisi zake leo Oktoba 4,2023Jijini Dodoma pamoja na Mpango Mkakati wake wa mwaka 2023-2025 ambapo Mgeni Rasmi katika uzinduzi huo alikuwa Balozi wa Sweden nchini Tanzania Ms. Charlotta Ozak.


Akizungumza kabla ya uzinduzi huo Rais wa (UTPC ), Deogratius Nsokolo amesema kuwa nchi ya Sweden imekuwa msaada mkubwa katika kuhakikisha tasnia ya habari nchi inaendelea kuimarika.

Rais huyo amesema moja kati ya mchango uliofanywa na nchi hiyo ni pamoja na vifaa vya kufanyia kazi vya kisasa kama komputa

Aidha ameongeza kuwa mpango mkakati wa UTPC ni kukuza uwezo wa kitaaluma wa wanahabari nchini, uhuru wa kupata taarifa na habari, kuhakikisha klabu za waandishi zinafanya kazi kwa ufanisi kwa kuweka mifumo mizuri na dhabiti ya usimamizi pamoja na kuhakikisha ulinzi na usalama wao na maslahi vinazingatiwa na UTPC kuwa na mifumo mizuri inayochangia shughuli zake zinakua kwa ubora zaidi.

“Tunafahamu jukumu letu muhimu kama waandishi wa habari ni kuleta mabadiliko chanya kwa jamii yetu, hasa kwa kuwa sekta ya habari ina jukumu kubwa katika kutoa habari za ukweli na kuijenga jamii yenye taarifa na maarifa ili iweze kufanya maamuzi sahihi”amesema.

Kwa upande wa mwakilishi kutoka serikalini Zamaradi Kawawa amesema kuwa wizara ya habari mawasiliano na teknolojia ya habari inawapongeza UTPC kwa kuimarisha sekta muhimu ya habari nchini pamoja na kuwa taasisi ya kwanza ya sekta ya habari kuhamia Dodoma.

“Hii inaonyesha ni kwa namna gani mmekuwa tayari kuunga mkono juhudi na maelekezo mbalimbali ya serikali yetu, tunawakaribisha taasisi nyingine za sekta ya habari kuja Dodoma kwasababu hii ndio makao makuu ya serikali lakini vilevile naomba niwapongeze kwa hatua nzuri ya kuandaa mkakati mpya wa kuhakikisha kwamba unaipeleka UTPC kwenye hatua nyingine na nawashukuru pia wadau wote ambao wamewezesha UTPC kufikia hatua hii”

“Tunawategemea UTPC kwa kuwa nyinyi mpo nchi nzima na tumekuwa tukifanya kazi kwa karibu na nyinyi na tuna amini changamoto zote wanapitia wana habari tunazipata kupitia nyinyi na taasisi nyingine lakini nyinyi mpo kona zote za taifa letu,”amesema Zamaradi.

Akiongea kwa niaba ya viongozi wa vilabu vya waandishi wa habari nchini mwenyekiti wa Chama cha waandishi wa habari Mwanza Edward Soko amesema kuwa UTPC ina msaada mkubwa kwa waandishi hivyo ni jukumu la kila mtu kuhakikisha inasimama vyema na kuweza kufikia malengo waliyo jiwekea.

Shughuli hiyo pia imeambatana na maonyesho ya gari maalumu linalotumia gesi lililotengenezwa na kampuni ya Scania pamoja na kuelezea mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mika 60 ya ushirikiano baina ya Sweden na Tanzania tangu mwaka 1963-2023.

Tags

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)