HALMASHAURI YA WILAYA YA TANGANYIKA YAZALISHA ZAIDI YA 25% YA MBEGU BORA ZA PAMBA NCHINI.

MUUNGANO   MEDIA
0

 

Kaimu Mkuu Bodi ya Pamba Tanzania James Shimbe akiongea na wadau wa pamba wilayani Tanganyika-.Picha na Mary Baiskeli.
Baadhi ya wadau wa pamba wakiwa kwenye kikao cha kujadili Maendeleo ya zao hilo wilaya ya Tanganyika-.Picha na Mary Baiskeli.

Mary Clemence, Katavi.

Bodi ya pamba Tanzania   imeanza mchakato wa kuirasimisha Halmashauri ya wilaya ya Tanganyika kuwa kitalu cha uzalishaji mbegu bora za pamba ili kuwasaidia wakulima kuzipata kwa urahisi na kwa bei nafuu.


Kaimu Mkurugenzi Mkuu Bodi ya Pamba Tanzania James Shimbe amebainisha hayo  kwenye kikao cha  wadau wa pamba cha kujadili maendeleo ya zao hilo kilichofanyika wilayani humo.


Shimbe amesema wamefikia hatua hiyo kutokana na Halmashauri  hiyo  kupiga hatua kubwa katika uzalishaji wa  mbegu bora za pamba nchini.


“Zinafuata utaratibu unaosimamiwa na ASA, TOSIC  na TARI wasimamizi  tasnia  ya pamba nchini, elimu inaendelea kutolewa  wakulima wazalishe kwa tija,  awamu hii  mmezalisha zaidi ya asilimia 25”amesema Shimbe akaongeza.


“Mwaka jana mmezalisha kilo milioni nne na laki mbili kwa musimu wa 2020/2022 na 2023 hadi kufikia sasa  mmezalisha kilo milioni tano  laki tatu na themanini ni uzalishaji mzuri,”


Msimamizi wa shamba  la Kilimi Nzenga mkoani Tabora la Wakala wa mbegu bora za kilimo (ASA) Jacob Chiwanga amesema wanayo mashamba 18 nchini yanayotumika kuzalisha na kusambaza.


“Tanganyika tuna shamba Luhafwe jipya ni sehemu mhimu tunayotarajia kulima mbegu, mchakato unaendelea wa kufungua shamba na kuzalisha tuongeze wigo wa usambazaji ukanda huu,”amesema Chiwanga.


Mratibu wa utafiti  zao la pamba kitaifa kutoka TARI Ukiriguru jijini  Mwanza Dakta  Paul Saidia amesema tija ya uzalishaji wa pamba nchini ni ndogo.


“Mkulima anavuna  kilo mia tatu hadi mia nne kwa ekari moja, Katavi tija ipo juu kidogo kutokana na maeneo yalivyo wanapata kilo 800 hadi 900,”


“Mbegu iliyogunduliwa na TARI, UKM68  tija yake inaanzia kilo 1200  kwa ekari moja, tumebaini  ugonjwa wa vuvuzali unaoathiri zaidi mimea, tatizo hili Katavi ni dogo sana,”amesema Saidia.


Mkulima wa pamba wa kijiji cha Majalila Abdallah Kakoso amesema utaratibu wa kuwa na kitalu cha kuzalisha mbegu  utakuwa na manufaa kwa wakulima.


“Mbegu zitapatikana kwa wingi na   kwa urahisi zaidi,lakini pia bei itapungua,  awamu hii kilo moja nasikia inauzwa sh 1400 mfuko mmoja sh 28,000 na zinatoka mbali,”“Wapo wakulima 


"wanaohitaji kulima lakini wanashindwa kumudu gharama,tunaishukru serikali kwa hatua hiyo tutaongeza uzalishaji,”amesema Kakoso.


Naye Mkuu wa wilaya ya Tanganyika Onesmo Buswelu   amewasisitiza watalaam kuhakikisha wanawasimamia wakulima waongeze uzalishaji na   ubora unaokidhi vigezo.


“Mhe.rais Samia Suluhu ameweka  nguvu kubwa ili tupate fedha za kigeni tuongeze dola katika nchi yetu pamba inapouzwa nje, hivyo tuzalishe kwa tija,”amesema Buswelu.


Kutokana na ongezeko la wakulima wa zao la pamba wilayani Tanganyika kiwango cha usambazaji mbegu kimeongezeka kutoka kilo 500 za awali  hadi kufikia zaidi ya kilo 500.


Tags

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)