OR-TAMISEMI, Tanga.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Angellah Kairuki ameagiza wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kusimamia ipasavyo ujenzi wa miundombinu ya kidato cha tano inayotakiwa kukamilika mapema mwezi Agosti, 2023.
Waziri Kairuki ametoa agizo hilo Julai 6, 2023 wilayani Korogwe wakati akizungumza na uongozi wa Mkoa wa Tanga wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani humo.
"Kila mmoja kwenye kituo chake cha kazi ahakikishe ujenzi wa miundombinu ya Elimu inakamilika, wanafunzi wetu watakapofungua shule Agosti,2023 wakute kila kitu kimekamilike na waanze masomo yao katika mazingira bora,"amesema.
Amesema Mhe. Rais Samia Suluhi Hassan ametoa fedha kwa kila halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya Elimu hususani ni ile ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha Tano wanaofungua shule Agosti 13, 2023 hivyo kila Mkurugenzi ahakikishe miundombinu hiyo imekamilika na ruhusa za kutoka nje ya kituo zinaweza kuanza Agosti 20, 2023 wanafunzi wakiwa wamesharipoti na kuanza masomo yao.

