WAHUDUMU WA AFYA NGAZI YA JAMII 1,322 WAJENGEWA UWEZO KUKABILIANA NA UGONJWA WA MARBURG.

0

  


 Dkt. Tumaini Haonga Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma, Wizara ya Afya. 



Dkt. Issessanda Kaniki Mganga Mkuu Mkoa wa Kagera.



Baadhi ya Wahudumu wa Afya ngazi ya jamii katika Kata ya Maruku  wakijadili namna ya utekelezaji wa utoaji wa elimu ya  ugonjwa wa Marburg baada ya kupewa mafunzo wakiwa sambamba na wawakilishi kutoka Wizara ya Afya pamoja na Red Cross Society.

Mmoja wa Wahumu wa Afya ngazi ya Jamii kutoka Kata ya Maruku  akionesha namna nzuri ya Unawaji wa mikono baada ya kupata Mafunzo ya kuwajengea uwezo kutoka Wizara ya Afya ,nyuma yake ni watumishi kutoka Red Cross Society .



Baadhi ya Magari ya Matangazo yenye ujumbe usemao "Jikinge na Marburg,Iweke Jamii yako Salama;Mtu  ni Afya ,Afya Yangu, Wajibu Wangu, Piga 199 Bure "yaliyofungwa Muziki unaotoa ujumbe wa tahadhari ya Kujikinga na  ugonjwa wa Marburg .

Mwakilishi kutoka ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa Jackline Saulo akikabidhi bango la uelimishaji kwa Mkuu wa gereza la Bukoba , pembeni yake ni mwakilishi kutoka Wizara ya Afya Beauty Mwambebule.


Wawakilishi kutoka Wizara ya Afya, Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma , ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa wakiwa katika picha ya pamoja katika gereza la Bukoba  baada ya kutoa elimu ya ugonjwa wa Marburg.


Baadhi ya Wavuvi katika ufukwe wa Igabilo Bukoba  wakipatiwa vipeperushi vinavyohusu elimu ya ugonjwa wa Marburg.


Baadhi ya wananchi  Bukoba wakifuatilia kwa makini vipeperushi  vya elimu ya ugonjwa wa Marburg .


Mwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Beauty Mwambebule akitoa elimu ya kujikinga ugonjwa wa Marburg katika shule ya Msingi Kilaini.


Na.Elimu ya Afya kwa Umma.

 

Katika kukabiliana na Ugonjwa wa Marburg ulioripotiwa rasmi mnamo tarehe 21 Machi, 2023 mkoani Kagera, Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara zingine za Kisekta pamoja na Wadau mbalimbali inaendelea kutekeleza mikakati ya uelimishaji na uhamasishaji jamii ikiwa ni pamoja na kuwajengea uwezo  Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii  1,322 katika Mitaa, Vijiji na Vitongoji vyote vya Halmashauri ya Bukoba Vijijini na Manispaa ya Bukoba. 

 

Hayo yamebainishwa leo April 8, 2023 katika Manispaa ya Bukoba Mkoani Kagera na  Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma ,Wizara ya Afya Dkt. Tumaini Haonga wakati  akizungumza katika mwendelezo wa utoaji wa elimu  ya afya kuhusu kinga na tahadhari dhidi ya Ugonjwa huo.

 

“Kupitia Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma, Serikali imetekeleza mikakati mbalimbali ili kuzuia ugonjwa huu usienee maeneo mengine nchini. Ili kuwafikia wananchi  mahali ambapo wanapatikana, Serikali inawatumia Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kwa kuwajengea uwezo wahudumu wapatao 1322 ambapo kati yao Wahudumu wanatoka Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba na Wahudumu wanaobaki wanatoka katika Halmashauri ya Bukoba Vijijini” amesema.

 

Dkt. Haonga amesema sambamba na kuwatumia Wahudumu wa Afya ngazi ya Jamii katika kutoa elimu ya afya katika maeneo mbalimbali, Serikali pia imetoa magari 8 maalum ya matangazo kwa ajili ya utoaji wa elimu ya Ugonjwa wa Marburg katika maeneo mbalimbali hususan sehemu zenye mikusanyiko.

 

“Utoaji wa magari haya 8 ni kuweka wigo mpana zaidi wa kuelimisha na kuhamasisha wananchi kupata uelewa na kuzingatia njia za tahadhari dhidi ya ugonjwa huu”amesema Dkt. Haonga.

 Dkt. Haonga ameendelea kufafanua kuwa katika kuendelea kuelimisha jamii, makundi muhimu wakiwemo viongozi wa dini wamepewa kipaumbele katika suala la uelimishaji ambapo hadi kufikia Aprili 6, 2023 takribani viongozi wa dini  310 walijengewa uwezo mkoani Kagera kutoka Taasisi mbalimbali za Dini .

 

“Kwa kushirikiana na Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF), Shirika la Tanzania Interfaith Partneship (TIP) na Uongozi wa Mkoa  tumeweza kuwafikia viongozi wa dini 310 kwa ajili ya kuwajengea uwezo sambamba na hilo tunaendelea kutoa vielelezo vya elimu kuhusu ugonjwa wa Marburg” amesema.

 

 Katika uelimishaji kwa Taasisi za Umma Dkt. Haonga karibu shule zote zimeweza kufikiwa pamoja Taasisi zingine ikiwemo magereza, sehemu za Ulinzi na Usalama ikiwemo jeshini na vielelezo vyote vya kutolea elimu vimekuwa vikitolewa kwenye taasisi hizo ambapo Chama cha Msalaba Mwekundu Tanzania (Tanzania Red Cross Society) kimekuwa kikishirikiana na Wizara ya Afya katika utoaji wa elimu ya afya kwa umma.

 

Kwa upande wake Mganga Mkuu Mkoa wa Kagera Dkt. Issessanda  Kaniki amesema baada ya kuunganisha nguvu kwa Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia Majanga, Wizara ya Maendeleo ya Jamii pamoja na Wadau pamekuwa na matokeo chanya katika suala la uelimishaji.

 

“Baada ya kuunganisha nguvu kupitia Wizara yetu ya Afya ,Wizara zingine za Kisekta pamoja na wadau mbalimbali mwitikio ni mkubwa ,watoa huduma ngazi ya jamii kwa kushirikiana na Tanzania Red Cross Society (TRCS) wameendelea kufikia jamii katika maeneo tofauti, hivyo nitumie nafasi hii kuwaomba wananchi wa Kagera waendelee kutoa ushirikiano kwa kuzingatia njiq za kinga na tahadhari zinazoshauriwa kitaalamu”amesema.

 

Naye Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kagera, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji, Thomas Fussy amesema wataendelea kushirikiana na jitihada zinazofanywa na Wizara ya Afya za kuhakikisha wageni wote wanaowahudumia wanazingatia kanuni za afya  ikiwemo kuhamasisha wananchi kunawa mikono mara kwa mara.

 

“Mkoa wa Kagera una mipaka saba, kupitia elimu tuliyopewa na Wizara ya Afya kupitia Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma, tutaisambaza katika sehemu mbalimbali tunazotoa huduma ikiwa ni pamoja na sehemu za mipakani hivyo tunaipongeza sana Wizara ya Afya kwa kujidhatiti katika kutoa elimu kila mahali “amesema.

 

MWISHO.

 

Tags

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)