HALMASHAURI TULILENGA KUCHANJA WATOTO 29,000 KAMPENI YA ELIMU NA HAMASA YA CHANJO YA SURUA IMEPAISHA HADI WATOTO 43,384-MKURUGENZI MPIMBWE.

MUUNGANO   MEDIA
0

Na.Elimu ya Afya kwa Umma.

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Mpimbwe Catherine Mashalla  ameishukuru Wizara ya Afya kwa kuweka nguvu katika suala la elimu na uhamasishaji wa chanjo ya Surua kwani hatua hiyo imesaidia kuvuka lengo la Halmashauri ambapo walikuwa na lengo la kuchanja watoto 29, 000 lakini kutokana na hamasa hiyo  wamechanja watoto  43,384.

Amebainisha hayo  Wilayani Mlele Mkoani Katavi wakati wa kuhitimisha kampeni ya siku 14 ya Elimu na Uhamasishaji wa chanjo ya Surua iliyoendeshwa kwa njia ya magari na njia ya simena iliyoanza Febururi 24.2023 hadi Machi 9 2023 ikiwa ni utekelezaji wa kampeni hiyo.

“Nina shukuru sana kama Halmashauri tumepata Support ya kutosha kabisa kutoka Wizara ya Afya na kwa maana hiyo sasa tumeweza kufikia mafanikio haya hata ile trend ya kesi mpya nayo imeshuka leo tunazungumzia 56 kutoka mia na zaidi kuna maendeleo makubwa, wale wanaokwenda kulazwa sasa hivi tuna namba tu ya watu wawili, hata wale tuliowalenga halmashauri kuwachanja walikuwa ni 29,000  leo hii tunazungumzia  zaidi ya elfu arobaini na tatu ni mafanikio makubwa”amesema Mashalla.

Aidha, Mkurugenzi Mtendaji huyo wa Halmashauri ameomba nguvu kubwa iliyotumika  katika elimu  na hamasa ya chanjo ya  Surua itumike pia katika  uhamasishaji kwa jamii kuhusu masuala ya lishe ili kupunguza tatizo la udumavu na utapiamlo katika eneo halmashauri ya Mpimbwe na Katavi kwa Ujumla.

Mganga Mkuu Halmashauri ya Mpimbwe mkoani Katavi Martin Lohay amesema watu waliogundulika na maambukizi ya Surua katika halmashauri hiyo ni   1967 huku akiipongeza Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Mkoa pamoja na Wizara ya Afya kwa kusaidia katika utoaji wa elimu na hamasa ya chanjo ya Surua.

Ikumbukwe kuwa katika kampeni ya siku 14 ya Hamasa  ya chanjo na Elimu ya Surua Halmashauri ya Mpimbwe, jumla ya kaya 15,750 zilitembelewa, na magari ya matangazo na sinema kufika katika maeneo ya  Majimoto, Kibaoni, Chamalendi, Mbende,Mwamapuli, Kasansa, Usevya, Ikuba, na Mamba huku watoto waliopona Surua ni 1749 kati ya wagonjwa  1967 na waliofariki hadi sasa ni watoto 16.

Tags

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)