Na Mwandishi Wetu, Hispania
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro amefanya mazungumzo na Uongozi wa vilabu vya Atletico Madrid na Getafe vinavyoshiriki ligi kuu nchini Hispania (Laliga) kwa lengo la kuitangaza Tanzania hususani sekta ya utalii
Aidha, Dkt.Ndumbaro amefanya mazungumzo na Kilabu ya Real Valladolid inayomilikiwa na mchezaji wa zamani wa Kimataifa wa Brazil, Ronaldo De Lima ambapo Klabu hiyo inatarajia kupanda daraja ili kushiriki Laliga
Dkt. Ndumbaro amebainisha hayo leo Jijini Madrid alipokutana kwa nyakati tofauti na viongozi wa Vilabu hivyo vya mpira vinavyoangaliwa na mamilioni ya watazamaji duniani.
Katika mazungumzo hayo amesema kuwa Viongozi wote wa Vilabu wameonesha utayari wa kushirikiana katika kuitangaza Tanzania kiutalii.
Akifafanua mazungumzo hayo Dkt.Ndumbaro amesema hiyo ni moja ya jitihada za kuhakikisha vivutio vya Utalii vya Tanzania vinajulikana duniani kupitia michezo kwa kutangazwa kupitia matangazo ya jezi ya Vilabu hivyo pamoja na mbao za matangazo (billboards) zilizopo uwanjani
" Shabaha yetu kubwa kama nchi ni kuhakikisha tunafungamanisha utalii na michezo kwa kutumia timu kubwa za mpira kwa lengo la kuwavutia watalii wengi zaidi kuja nchini Tanzania" amesisitiza Dkt.Ndumbaro
Ameongeza kuwa Tanzania inategemea utalii wake wa Wanyamapori kwa asilimia 100 hivyo kupitia mkakati wa kutumia michezo vivutio vingine vya utalii kama vile utalii wa fukwe, utalii wa utamaduni pamoja na utalii wa ikolojia utaweza kujulikana dunia kote na kuwa chachu ya watalii wengi kuanza kumiminika nchini Tanzania.
Katika mazungumzo hayo Ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Uhispania mwenye makazi yake mjini Paris, Ufaransa, Samwel Shelukindo
Mwisho.