Na Avelina Musa - Dodoma.
Katibu wa NEC,Itikadi,Uenezi Na Mafunzo CPA Amos Makalla ametangaza Majina ya waliopenya kwenye uteuzi wa awali uliofanywa na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa katika kikao kilichofanyika julai 28,mwaka huu Jijini Dodoma.
Akisoma majina hayo CPA Makala ameyataja majina 7 ya wagombea wa Jimbo la Arusha Mjini waliopita katika mchujo huo akiwemo Mhe.Paul christian Makonda huku Mpinzani wake Mhe. Mrisho Gambo ambaye pia anamaliza muda wake wa ubunge jimboni Arusha akiwekwa nje ya mtanange huo, akitaja majina hayo katika jimbo la Arusha Mjini amesema walioteuliwa ni Ndugu Ally Said Babu,Ndugu Hussein Omarhajji Gonga,Ndugu Aminatha Salash Toure,Ndugu Mustapha Said Nassoro,Ndugu Paul Christian Makonda, Ndugu Lwembo Mkwavi Mghweno na Ndugu Jasper Augustino Kishumbua.
Hayo yamejiri Leo julai 29,2025 katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi Jijini Dodoma wakati akitangaza majina ya wagombea walioteuliwa kwenda hatua inayofuata ya kura za maoni ambapo pia amesema idadi ya wagombea majimboni ni zaidi ya wagombea (5,000) na kwa nafasi za Udiwani ni zaidi ya wagombea (30,000)
Hata hivyo amewataka wagombea walioshindwa kupenya kwenye mchujo huo kuwa watulivu na kuendelea kutoa ushirikiano kwa kuwa chama hicho bado kina nafasi za kutosha.
"Kwa wale ambao hawatapata nafasi niwaombe kuwa watulivu,waendelee kutoa ushirikiano ndani ya Chama Cha Mapinduzi wameonyesha kwamba ni wanachama wazuri na wametimiza haki yao ya kikatiba ya kuomba ridhaa,"
Makalla ameendela kusema "endapo hutopata nafasi kwa uteuzi huu ambao nitautangaza basi muendelee kutoa ushirikiano Chama Cha Mapinduzi kina nafasi nyingi,inawezekana leo ukakosa Udiwani ukakosa Ubunge lakini zipo nafasi nyingi ndani ya Chama Cha Mapinduzi." Amesema CPA Amos Makalla
Aidha amewapongeza wanachama wa Chama Cha Mapinduzi kwa kujitokeza kuchukua fomu ili kuwania nafasi mbalimbali za Udiwani Viti Maalum,Uwakilishi katika majimbo ya Zanziba,Ubunge na Ubunge wa Viti Maalum
Ikumbukwe kuwa mchakato huu ulipangwa kufanyika mapema julai 28,2025 lakini zoezi hilo halikufanikiwa kutokana na mchakato huo kuhitaji muda mwingi zaidi ili kutekeleza kwa mafanikio sambamba na kutenda haki kwa kila aliyestahili.
