MBIO ZA MWENGE, WAZIRI JAFO AHIMIZA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

MUUNGANO   MEDIA
0



 Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe.

Dkt. Selemani Jafo ameendelea kuhimiza matumizi ya nishati safi ya

kupikia ili kukabiliana na uharibifu wa mazingira kutokana na ukataji wa

miti.

Ametoa rai hiyo alipokuwa akizungumza na Shirika la Utangazaji la

Zanzibar (ZBC) wakati wa uzinduzi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa

2024 katika Uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi mkoani Kilimanjaro

uliofanywa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa leo Aprili 02, 2024.

Dkt. Jafo amesema kuwa Serikali ilitangaza kusitisha matumizi ya kuni na

mkaa kwa taasisi zinazolisha watu zaidi ya 100 kuanzia Januari 2024

ambapo tayari taasisi hizo zimetekeleza maelekezo hayo.

Amesema kuwa kila mwaka takriban hekta laki nne za misitu zinapotea

kutokana na kukatwa kwa ajili ya kuni na mkaa hivyo Serikali

inahamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuinusuru.

“Utunzaji wa mazingira unagusa mambo mengi, hivi karibuni Rais wa

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu

Hassan alizindua Kampeni ya Nishati Safi ya Kupikia ili kuhifadhi

mazingira,“ amesisitiza.

Aidha, Waziri Jafo amesema kuwa Mwenge wa Uhuru mwaka huu

umeleta faraja kubwa katika utunzaji wa mazingira kwani utakimbizwa

mikoa yote hivyo utasaidia wananchi kuelewa dhana nzima ya utunzaji

wa mazingira na changamoto kubwa kwa sasa ni utunzaji wa mazingira

Itakumbukwa kuwa katika kilele cha Mwenge wa Uhuru 2023

kilichofanyika Oktoba 14 mkoani Manyara, Makamu wa Rais wa Jamhuri

ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango alitoa rai kwa Ofisi

ya Waziri Mkuu kuendelea kutumia ujumbe unaohamasisha jamii utunzaji

wa mazingira ili kusaidia kulinda na kutunza Mazingira.

Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024 una kaulimbiu "Tunza Mazingira na

Shiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa Ujenzi wa Taifa Endelezu"

ambayo inaweka msisitizo kwa namna nyingine katika uhifadhi wa

mazingira.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)