M/RAIS AANZA ZIARA MKOANI TANGA

MUUNGANO   MEDIA
0



 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. Philip

Mpango ameigiza Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na uongozi

wa mkoa wa Tanga kuchukua hatua za mapema katika kukabiliana na

changamoto ya soko la matunda yanayozalishwa mkoani humo.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati akizungumza na Wananchi wa

Kabuku Wilaya ya Handeni akiwa ziarani mkoani Tanga leo tarehe 21 Februari

2024. Ameuagiza uongozi wa mkoa wa Tanga kufanya tathimini na kutambua

kiasi cha matunda yanayozalishwa katika eneo hilo.

Aidha Makamu wa Rais amemuagiza Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara

kukutana na wamiliki wakubwa wa viwanda vya kuchakata matunda

(Bakhresa na Jambo Product) ili waweze kutumia matunda yanayozalishwa

Wilaya ya Handeni na Tanga kwa ujumla katika bidhaa zao.

Halikadhalika Makamu wa Rais amewasihi wananchi wa Kabuku na

Watanzania kwa ujumla kuongeza jitihada katika utunzaji wa mazingira ili

kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi. Amesema athari za

uharibifu wa mazingira zimepelekea ongezeko la joto kupita kiasi, ongezeko la

mvua ambayo imepelekea uharibifu wa miundombinu na mlipuko wa

magonjwa.

Amesema ni muhimu watanzania kutambua uhifadhi ya mazingira ni jukumu

la kila mmoja kwa kuacha kukata miti ovyo, kuacha kuchoma misitu pamoja

na kupanda miti na kuitunza.

Makamu wa Rais amewasisitiza wananchi wa Kabuku kuhakikisha

wanazingatia elimu kwa watoto ili kuwa na kizazi bora na chenye maarifa kwa

manufaa ya Taifa. Pia amewaasa wananchi wa eneo hilo kuzingatia lishe kwa

kuwa ndio msingi wa afya bora ya mwili na akili.

Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema Wizara imepokea shilingi bilioni 25

kwaajili ya ujenzi wa mradi mkubwa wa kutoa maji eneo la Segera hadi

Kabuku mkoani Tanga kwa lengo la kukabiliana na adha ya upatikanaji wa

maji katika eneo hilo. Waziri Aweso amesema mradi huo unatarajia kukamilika

mwanzoni mwa mwaka 2025 ambapo tayari mkandarasi anaendelea na kazi.

Aidha Waziri Aweso ametoa wito kwa mkandarasi kuhakikisha anafanya kazi

na kukamilisha kwa wakati pamoja na kuwashirikisha wananchi na viongozi

wa eneo husika wakati wote wa ujenzi wa mradi huo. Aidha ameahidi kwamba

Wizara ya Maji itahakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati kama

ilivyopangwa.


Kwa upande wake Naibu Waziri wa TAMISEMI Deogratius Ndejembi amesema

tayari Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) imepokea shilingi bilioni

30 ambazo zitaanza kushughulikia changamoto mbalimbali za barabara hapa

nchini. Ameongeza kwamba kwa upande wa Wilaya ya Handeni, Serikali tayari

imetenga fedha kwaajili ya ujenzi wa barabara ya Sindeni – Kwedikazo ya

kilometa 37.7 kwa kiwango cha lami. Amesema katika Wilaya hiyo TARURA

itaanza mchakato mara moja wa kuhakikisha barabara zilizoharibiwa na mvua

zinatengenezwa ili ziweze kupitika vema.

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais

21 Februari 2024

Tanga.

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)