SERIKALI YAJA NA MFUMO WA KUPOKEA NA KUCHAMBUA MWENENDO WA MAJANGA NCHINI.

MUUNGANO   MEDIA
0

       

Na. Gideon Gregory, Dodoma.

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Ummy Nderiananga amesema kuwa serikali kwa kushirikiana na wadau imekuja na mfumo wa kuweka vifaa vya teknolojia ya mawasiliano kwa kupokea na kuchambua mwenendo wa majanga nchini.

 

Mhe. Nderiananga ameyabainisha hayo leo Oktoba 13,2023 Jijini Dodoma wakati akifungua kongamano la maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kupunguza madhara ya maafa inayoenda sambamba na kauli mbiu isemayo “Imarisha usawa kwa uthabiti endelevu.

Aidha amesema kuwa wameanzisha jukwaa la kijamii la kidigitali la mawasiliano ambapo wananchi wanaweza kupokea taarifa za tahadhari za mapema kuhusu maafa au kupewa taarifa bure kuhusu maafa katika eneo lolote.

 

“Kwa mfano wenye simu zenu hapa sasa hivi, unaweza kuchukua simu yako ukaandika *190# utaona mwenyewe itakupeleka karibu Ofisi ya Waziri mkuu inakuuliza umepatwa na changamoto gani pengine kama ni ajali au mafuriko au mengineyo unaeleza kila kitu hapo ili kwa pamoja tuweze kufanya kazi kwa pamoja na kwa haraka,”amesema Mhe. Nderiananga.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mwandamizi wa World Vision Tanzania Dkt. Joseph Mayala amesema kuwa wao shirika la kimataifa wanahakikisha viongozi wa dini wanashirikishwa katika mikakati yote inayohusiana na suala la kukabiliana na maafa nchini kwani wana ushawishi mkubwa katika jamii.

 

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Manejimenti ya Maafa (RAPID) Taniel Mkongo amesema kuwa kauli mbiu ya leo katika maadhimisho hayo inatokana na mkakati wa sendai wa kupunguza madhara ya maafa wa 2015-2030 ambao unataka kushughulikia sababu za msingi za madhara ya maafa.

 

“Tunajua kuwa mara nyingi watu maskini na walio hatarini zaidi wanapata athari kubwa za maafa na wanakabiliwa na athari kubwa zaidi, kupambana na kutokuwiana ni sehemu muhimu ya kujenga mustakabali wa kustahimili kupunguza athari za maafa,”amesema.

 

Siku ya kimataifa ya kupunguza maafa ilianza mwaka 1989 baada ya wito kutoka kwa Baraza la Umoja wa Mataifa kutaka kuwepo kwa siku hii maazimio Na. 64/200  Desemba 21,2009 ilinayohitaji watu na jamii zote duniani kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kudhibiti madhara ya maafa.

 

Chapisha Maoni

0Maoni
Chapisha Maoni (0)