Naibu Waziri Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe (Mb) amemuhakikishia mwekezaji wa kiwanda cha TROLLE MEES LE TANZANIA IVS LTD soko la uhakika la mafuta ya mawese baada ya kuanza utekezaji wa kutatua changamoto zilizojitokeza kwenye ziara ya Mhe Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Mhe Kigahe ameyasema hayo Machi 26, 2023 Mkoani Kigoma wakati wa kupokea taarifa ya kamati ya kufanya tathimini ya changamoto zilizojitokeza katika kuongeza thamani ya zao la mchikichi mkoani Kigoma.
Akiwa mkoani Kigoma tarehe 27 Februari ,2023 Mhe. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa (Mb) alipokea changamoto anuai kutoka kwa mwekezaji anaejenga kiwanda cha kuchakata na kuongeza thamani mafuta ya mawese cha TROLLE MEES LE TANZANIA IVS LTD kinachomilikiwa na Bw. Abdalah Mwilima.
Aidha changamoto zilizoainishwa na mwekezaji huyo ni pamoja na upungufu malighafi ya zao la mchikichi, Eneo la kupanda zao la mchikichi na umeme kutokuwa na nguvu ya kutosha kuendesha mitambo iliyofungwa kiwandani hapo, Kutopata kiasi chote cha mkopo alichoomba katika benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB).
Kutokana na changamoto hizo, Mhe Waziri Mkuu aliagiza Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kupitia taasisi zake ikiwemo SIDO kushughulikia changamoto zote zilizoanishwa na kuzipatia ufumbuzi kwa wakati.
Akizungumza wakati wa kupokea taarifa ya kamati hiyo Mhe. Kigahe amemuhakikishia mwekezaji huyo kuwa Wizara imepokea changamoto zote zilizoanishwa na kuzifanyia kazi kwa haraka huku baadhi zikiwa zimepatiwa ufumbuzi tayari na zingine zikiwa bado kufanyiwa kazi.
“Nikuhakikishie changamoto zote tumeanza kuzifanyia kazi baada ya kupokea maelekezo ya Mhe. Waziri Mkuu Benki ya Maendeleo ya kilimo (TADB) imeshafanyia kazi changamoto ya kifedha, kuhusu changamoto ya umeme tumeongea na Meneja wa Tanesco Mkoa wa Kigoma anafanyia kazi kwa uharaka zaidi" Alisema Mhe. Kigahe
Katibu Mkuu Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt. Hashil Abdallah amemhakikishia Naibu Waziri utekelezaji wa changamoto zilizoanishwa kwa kusema kuwa, atahakikisha zao la mchikichi linawakwamua Wananchi wa Mkoa wa Kigoma kwa kuwa ndilo zao la kimkakati.